MBINU 5 ZA KUJIHAMI NA
KUPAMBANA NA MAJARIBU
1. 1. KESHA UKITAMBUA UDHAIFU
WAKO
Kesheni, mwombe, msije mkaingia
majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu (Math 26:41)
Mlinzi aliye makini anajua anapaswa
kukaa chonjo kulinda maeneo dhaifu ambayo adui anaweza kuyatumia na
kumuingilia. Miili yetu ina nyufa za udhaifu. Japokuwa udhaifu wa miili
haufanani. Udhaifu wako unaweza kuwa sio udhaifu wa wenzako.
Jaribu moja linaweza kuwangukia watu
wawili, lakini wakatofautiana kuhisi uzito wake kulingana na maumbile ya
kihaiba au historia ya kiroho ya kila mmoja wao. Hivyo jichunguze. Kama kitendo
cha kunusa harufu ya sigara, kusikia muziki wa lege, kugusa kiganja cha mpenzi,
au kutazama filamu, kinaamsha hisia au kumbukumbu fulani---inayokusukumia uvuke
mstari mwekundu, basi tambua hilo haraka na urudi nyuma kwa usalama wako. Mtume
Paulo anatoa ushauri huo huo kwa kijana Timotheo, akimwambia, “zikimbie tamaa
za ujanani” (2Tim 2:22). Na tena tunahimizwa na mtume, “tuweke kando kila mzigo
mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi” (Waeb 12:1.) Unapotambua udhaifu
wako jihadhari nao kwa kutobakia katika mazingira hatarishi kwa usalama wako.
Ni muhimu mno kuzingatia tahadhari
hiyo. Bora kuwa mwoga wa kukimbia dhambi inayokuotea mlangoni na ukaishia
kuishi siku nyingi kama kunguru, kuliko kuwa jasiri wa kumkaribia chatu na kufa
mapema kipumbafu kabla ya siku zako. Ni salama kutembea katikati ya njia kuu na
kufurahia ujana wako kwa kitambo kirefu, kuliko kuchepuka njia za mkato
ukaishia kugongwa na nyoka wenye sumu. Afadhali ufahamu udhaifu wako mapema na
uchukue hatua za haraka kuudhibiti kabla haujadhulika.
2. FIKIRI MADHARA YANAYOWEZA KUKUPATA KWA
KUKUBALI USHAWISHI
Je! Mtu aweza kukanyaga makaa ya moto, Na
nyayo zake zisiungue? (Mith 6:28)
Ni ngumu kufikiria madhara ya
kishawishika Mjaribu anapokujia na ahadi nyingi. Anakwambia, kula tunda hili
nawe utafanana na Mungu. Kunywa kidogo nawe utasahau misongo ya umaskini wako.
Achia breki za uaminifu nawe ujimwage katika anasa. Ni hapo baadaye tu, baada
ya kuridhia, ndipo unapojiuliza, 'nimefanya nini?' Uzuri wa moto ni pale ukiwa
mbali.
3. JITAMBUE WEWE NI
NANI NA AMUA MAISHANI MWAKO LA MUHIMU NI LIPI
Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima,
akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja
na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo. (Waeb
11:24,25)
Dalili ya kuwa mtu mzima ni kujua
wewe ni nani na lipi la muhimu katika maisha yako. Musa alipoingia tu utu uzima
aljiitambua yeye ni nani. Kwa kujitambua kama mtoto wa Mungu na si wa farao
aliweza kuzikimbia anasa za ikulu na kukimbilia mateso pamoja na watu wa Mungu.
Upepo wa majaribu hauna nguvu kwa mtu anayejitambua na aliye na vipaumbele anayoyathamini maishani kabla ya vingine.
4. OMBEA WOKOVU DHIDI
YA MAJARIBU YANAYOKUKABIRI
Ombeni kwamba msiingie majaribuni
(Luk 22:40). Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni,….usitutie
majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. (Mat. 6:9,13)
Ombi la kupokea nguvu ya kustahimili
majaribu ni ombi ambalo Mungu anatamani kulijibu. Ndiyo maana Yesu alituwekea
ombi hiilo mdomoni mwetu akitutaka kila tusalipo tulitaje ili tupokee wokovu.
Na Yesu kwa kusema hivyo alijua kuwa, “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha
mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa
kutokea, ili mweze kustahimili.” (1 Kor 10:13). Na kwa kuwa Mungu anataka
kukusaidia katika mapambano yako dhidi ya majaribu, unapaswa uombe. Lakini,
omba ipi inayofika masikioni mwa Mungu?
Omba kwa bidii. Usimwombe Mungu kwa
kujaribu. Usim-beep ikiwa kama unashida naye ya dhati. Omba kama Eliya
alivyoomba kwa bidii mvua iliyozuiliwa miaka mitatu inyeshe (Yak 5:17; 1Waf
17). Mungu anataka kujua kama unamaanisha unachokiomba. Ukionesha bidii kwamba
unajali kupokea wokovu wake hakika utajibiwa. Maana, “Kuomba kwake mwenye haki
kwafaa sana, akiomba kwa bidii.” (Yak 5:16)
Pia omba kwa imani. Usiomwombe Baba
Mungu kama watoto wa mitaani wanavyoomba msaada kwa Wapita-njia. Tena, usiombe
kama manabii wa kishenzi (wa mungu Baali) wanaoomba wakijitaabisha ili mungu
wao aguswe na huruma na kuwaokoa (1 Waf 17). Ombea wokovu dhidi ya majaribu kama mwana wa nyumbani
anayetarajia kupokea zawadi njema kutoka kwa Baba anayejali (Luk 18:7). Omba
bila mashaka. Omba kwamba mapenzi ya Baba yatimizwe kwako; ukiamini kuwa,
“katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia
mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake” (War 8:28). Nawe kwa imani hiyo utaona mlima wa majaribu
uking’oka mbele yako na kuzama katika bahari ya kusahaulika (Mar 11:23)
5. SIFIA WEMA NA UWEZO WA MUNGU KWA NYIMBO NA
PAMBIO
Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya?
Na aombe. Ana moyo wa kuchangamka? Na aimbe zaburi. (Yak 5:13; linganisha na
Kol 3:16; Efe 5:19)
Zaidi ya kuomba kwa imani,
unapopatikana na changamoto, changamka katika sifa. Vaa uchangamfu wa
Yehoshafati umshinde adui yako (2Nyak 20:20,21). Imba nyimbo za ushindi ukaribisha ushindi. Imba nyimbo za Paulo na
Sila uuone wokovu wa Bwana kwa kishindo na tetemeko (Matendo 16:23-29). Kamwe
Mungu hatabakia kwenye kiti chake cha enzi ametulia, anawaangalia wanawe pasipo
kufanya kitu—wanawe wanaosifia Mungu wao masikioni mwa adui zao. Kamwe, Mungu
hatawaangusha watu wake wanaoshikiria imani yao kwake hata kwa kumuimbia. Na
kama wataanguka chini, siku ya tatu atawanyanyua toka mavumbini; maana,
hawastahili kuwepo hapo chini. Ita ushindi kwa nyimbo za sifa na shukurani,
“Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo.” (1Kor 15:57)
<<<<MUNGU AKUBARIKI SANA>>>>
MAOMBI NA MAOMBEZI
WASILIANA NA MCHUNGAJI LAURENT MPOMA
NCHI YA UKOMBOZI MINISTRY TANZANIA
(HUDUMA YA MAOMBEZI)
PIGA AU WHATSAP : +255762756542
0 Comments