Follow us

Kwanini ulaaniwe?

Tangazo



Kuna sababu nyingi tu zinazomfanya mtu au kitu kipokee laana. Sababu hizo ni kama zifuatazo:-

 LAANA YA KUJITAMKIA AU KUTAMKIWA KWA KUJUA AU PASIPO KUJUA.

Nianze na mfano kwanza; unakuta mtu anasema, “sisi ukoo wetu ni maskini tu hata tufanyaje”, “kwa hii kozi niliyosoma sijui kama nitapata kazi kwa kweli”, “watoto wa mama fulani hawaolewagi”, “mimi masomo ya sayansi hata nifanyaje siji kufaulu”, hiyo ni baadhi ya misemo iliyobeba laana ndani yake.

Na hakika lazima kuna nguvu itafuatilia kuhakikisha inatimiza makusudi yaliyopo ndani ya misemo hiyo. Na mara nyingi laana ya namna hii, watu wengi tunajitamkia pasipo kujua kuwa tunachokitamka kitatimia katika maisha yetu. (Warumi 12:14, Yakobo 3:9).

LAANA ITOKANAYO NA KUWALAANI WATUMISHI WA MUNGU WALIOBARIKIWA.

Kubali ukatae, mtu yoyote au kitu chochote Mungu alichokibariki mwanadamu hawezi kukilaani. Na ikiwa umemlaani au kutamka maneno mabaya juu ya mbarikiwa yoyote wa Mungu, laana hiyo inafanyika kuwa baraka kwa uliyemtamkia lakini inakurudia wewe kama laana (Hesabu 23:11 na Hesabu 24:10).

Hesabu 22:12. Mungu akamwambia Balaamu, usiende pamoja nao; wala usiwalaani watu hawa, maana wamebarikiwa.

 

Mwanzo 12:3. Nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.

Mwanzo 27:29b. Atakayekulaani alaaniwe, na atakayekubariki abarikiwe.

LAANA YA WAZAZI.

Hii unaweza ukaipata kutokana na jinsi unavyowatendea wazazi wako. Haijarishi wazazi wako ni watu wa namna gani au wamewahi kukukosea nini, watabaki kuwa wazazi wako na ni lazima uwape hushima yao (Kutoka 20:12). Kitu chochote kibaya utakachowafanyia au kuwasemea wazazi wako, Mungu atajilipishia kisasi katika maisha yako au hata uzao wako (Mathayo 15:4).

Mwanzo 9:24-25. Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea (alimchungulia na kuuona uchi wake). Akasema, na alaaniwe Kanaani; atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake.

Pasipo kujarisha wazazi wako wanatabia gani, laana yoyote watakayo itamka juu yako au manung’uniko yoyote utakayo wasababishia yatafanyika kuwa laana itakayo laani maisha yako.

Kumbukumbu la Torati 27:16. Na alaaniwe amdharauliye baba yake au mama yake. Na watu wote waseme, Amina.

Laana hii ni tofauti na nyingine, inahitaji upate kibali cha wazazi pia ili kuifuta katika maisha yako. Ikiwa hadi hapa, umetambua uko chini ya laana ya wazazi, huna budi kuwataka radhi kwa uliyowahi kuwakosea.

 

LAANA YA KUWANYANYASA WAGENI, YATIMA NA WAJANE.

Hii ni laana inayowapata watu kwa sababu ya tamaa ya mali, mara nyingi; anapofariki mume mwenye uwezo kifedha wa mwanamke fulani au baba mwenye uwezo kifedha wa watoto fulani ndugu wa marehemu wanaanza kuwanyanyasa mke na watoto wa marehemu kwa ajili ya kuwadhurumu mali na kuwazushia mambo kibao.

Kwa kosa hilo Mungu hujilipishia kisasi juu ya yoyote aliyehusika kufanya hivyo pasipo kujali kuwa unaowanyanyasa wanamjua au hawamjui Mungu, machozi yao ni kiberiti cha kuwasha hasira ya Mungu kwako. Kwani Mungu amesema yeye ni mume wa wajane na baba wa yatima (Yakobo 1:27, Zaburi 68:5).

Kutoka 22:21-24. Usimwonee mgeni, wala kumtendea jeuri; kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri. Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao, na hasira yangu itawaka moto, nami nitawaua ninyi kwa upanga; na wake wenu watakuwa wajane, na watoto wenu mayatima.

Kumbukumbu la Torati 27:19. Na alaaniwe apotoaye hukumu ya mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa nu mumewe. Na watu wote waseme, Amina.

LAANA ITOKANAYO NA KULA/KUIBA FUNGU LA KUMI LA MUNGU.

Laana hii imewafunika watu wengi sana makanisani, unakuta mtu anafanya biashara au ni mfanyakazi katika ofisi au shirika fulani lakini hana maendeleo yoyote, na wengine wanapokea mishahara mikubwa lakini fedha inapotea katika mazingira yasiyo na maelezo kamili.

 

Kama wewe ni mmoja wapo, amabaye huoni mafanikio licha ya fedha nyingi unayoipata, biashara yako haikui licha ya kuwa unaitangaza sana, tambua unatembea chini ya laana kwa kutotoa fungu la kumi.

Malaki 3:9. Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi (zaka-fungu la kumi), naam, taifa hili lote.

LAANA ITOKANAYO NA KUTENDA DHAMBI AU KUTOTII MAAGIZO YA MUNGU.

Mwanadamu anapofanya dhambi, hasira ya Mungu inawaka juu yake, na Mungu anaagiza laana juu ya mwanadamu huyo kwa makusudi ya kumkumbusha mwanadamu huyo kuwa anatakiwa kurejea kwa Mungu na kuziacha njia zake mbaya.

Mwanzo 3:17. Akamwambia Adamu, kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, usiyale (kutotii); ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako.

Kumbukumbu la Torati 11:26-28. Angalieni, naweka mbele yenu hivi leo baraka na laana; baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, niwaagizayo hivi leo; na laana ni hapo msiposikiza maagiza ya Bwana, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua.

LAANA ITOKANAYO NA KUMWAGA DAMU.

Watu wengi sana wanatembea na laana hii pasipo wao wenyewe kujua, kwa kuwaua watu (ili wapate mali na utajiri) au kwa kutoa mimba maisha yako yanalaaniwa. Ndiyo maana utawakuta wengine wana mali nyingi lakini hawana amani na wengine wamehangaika kila sehemu kutafuta watoto lakini hawapati, ni kwa sababu wamesahau damu waliyoimwaga miaka mingi iliyopita, damu ambayo bado inadai kisasi juu yao, mbele za Mungu.

Mwanzo 4:10-11. Akasema (Mungu), umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basa sasa umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako.

LAANA ITOKANAYO NA KUFANYA UZINZI NA MZAZI WAKO AU MZAZI WA MKE AU MUME (MKWE) WAKO AU NDUGU YAKO WA DAMU.

Laana hii huwapata wale wanaotimiza masharti ya waganga wa kienyeji hasa, ili kujipatia mali za kishirikina.

Kumbukumbu la Torati 27:20,22, na 23. Na alaaniwe alalaye na mke wa baba yake, kwa kuwa amefunua mavazi ya babaye. Na watu wote waseme, Amina. Na alaaniwe alalaye na umbu lake, binti ya babaye, au binti ya mamaye. Na watu wote waseme, Amina. Na alaaniwe alalaye na mkwewe, mamaye mkewe. Na watu wote waseme, Amina.

LAANA YA KUFANYA MAPENZI NA MNYAMA.

Ni kwa mtu yo yote aliyewahi kufanya mapenzi na mnyama kwa kutimiza masharti ya kishirikina na uchawi, kwa taama binafsi au kwa minajili ya kujipatia fedha, kwa mfano; mbwa, farasi n.k.

Kumbukumbu la Torati 27:22. Na alaaniwe alalaye na mnyama wa aina yo yote. Na watu wote waseme, Amina.

 

Kuna sababu au vitu vingi vinavyoweza kukusababishia laana katika maisha yako, kazi au biashara yako, ama vitu unavyovimiliki kama shamba au nyumba.

Na kitu kibaya zaidi ni kwamba laana inarithiwa, kutoka kizazi kimoja kwenda kinachofuata. Unaweza usione matokea ya laana katika maisha yako ya sasa na ukaamua kunyamaza ilihali ukijua kuna mambo uliwahi kufanya yanayofanana na hayo hapo juu. Nakuambia hiyo laana ni lazima ikufuatilie kama siyo wewe basi ni uzao wako, na kuna watu wanaishi chini ya laana zilizosababishwa na wazazi wao ambao unaweza ukakuta hawapo hai kwa sasa.

Kumbukumbu la Torati 28:45-46. Na laana hizi zote zitakujilia juu yako, zitakuandama na kukupata, hata uangamizwe, kwa kuwa hukusikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, kushika maagizo yake na amri zake alizokuagiza; nazo zitakuwa juu yako kwa ishara na ajabu, na juu ya uzao wako milele.

JE, UNAWEZA KUWA UMELAANIWA PASIPO WEWE KUJUA?

Hakika jibu ni ndiyo; unaweza kuwa ulifanya uovu au jambo lolote kati ya hayo yanayoweza kusababisha laana katika maisha yako, na bado hujaona matokeo ya hiyo laana katika maisha (labda uwe ulitubu na kuvunja laana hiyo), kinyume na hapo laana hiyo bado iko juu yako na inakufuatilia kama siyokukupata wewe basi ni uzao wako, kama tulivyoona kuwa laana inarithiwa (kumbukumbu la Torati 28:45-46).

NI VITU GANI VINAWEZA KULAANIWA?

Kwanza wewe mwenyewe unaweza kupokea laana katika mwili wako, vitu unavyomiliki kama ardhi, nyumba, mifugo n.k huweza kulaaniwa kwa ajili yako.

 

ARDHI. Unailima ardhi lakini hupati mazao kutoka kwake, unazingatia kilimo cha kisasa lakini mavuno ni haba.

Torati 29:27. Ndipo ikawashwa hasira ya Bwana juu ya nchi (ardhi) hii, kwa kuleta juu yake (ardhi) laana yote iliyoandikwa katika kitabu hiki.

UZAO WAKO. Watoto wako wanakuwa wasumbufu haijawahi kutokea; wana kiburi, wana tabia mbaya, umetumia upole na ukali kuwakanya lakini hawakusikii, au hata hawana mafanikio kwa kila jambo wanalolifanya.

Torati 28:18. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako.

MIFUGO YAKO. Unajitahidi kufuga mifugo kwa njia za kisasa, lakini mifugo haiongezeki, ikizaa watoto wanakufa, au kila siku unaibiwa wewe, mifugo yako inapotea pasipo kuonekana.

Torati 28:18. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako (mifugo yako).

Kazi za mikono yako na uchumi wako kwa ujumla. Unafanya kazi au biashara ambayo huoni faida yake, zaidi ya kukupatia fedha ya kujikimu tu. Umekuwa na uchumi ule ule miaka nenda rudi na ndiyo kwanza unazidi kushuka chini.

Torati 28:20. Bwana atakuletea laana na mashaka, na kukemewa katika yote utakayotia mkono wako kuyafanya (kazi na biashara zako), hata uangamie na kupotea kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo yako, uliyoniachia kwayo.

NYUMBA YAKO. Unaweza ukawa umejenga nyumba lakini huna furaha nayo, hutamani kuendelea kuishi ndani yake, unaona ni afadhari ukapange kuliko kuendelea kuishi ndani ya nyumba yako uliyoijenga au kuinunua kwa fedha yako mwenyewe.

Mithali 3:33. Laana ya Bwana i katika nyumba ya waovu, bali huibariki maskani ya wenye haki.

 

MWILI WAKO. Unapata magonjwa yasiyo na sababu, ukifuatilia chanzo cha magonjwa au wapi ulipata maambukizo hakuna unakoweza kupata jibu. Na hata ukienda hospitali bado hupati uponyaji.

2 Nyakati 7:13. Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni (magonjwa).

ANGA AU MBINGU. Mvua hainyeshi au hainyeshi kwa wakati. Maombi yako hayafiki mbele za Mungu, anga imefungwa isipitishe kitu chochote kwa ajili yako.

2 Nyakati 6:26. Ikiwa mbingu zimefungwa, hata hakuna mvua, kwa sababu wamekukosa wewe.

 

Hadi kufikia mwisho wa somo hili nina imani kuwa umetambua laana ni nini na ikiwa upo chini ya laana na hukujua, basi leo umefumbuliwa macho. Sitaki nikuache hivi hivi, nitafanya maombezi kwa ajili yako ili Mungu akurehemu na kukufungua vifungo vyote vya laana. Kwanza kabisa nataka nikuombe rehema na kisha nivunje na kufuta laana zote na kutamka baraka katika maisha yako.

Unachotakiwa kufanya ni kunipa ushirikiano ambao ni; unatakiwa kuwa na imani thabiti, kwani si mimi ninayetenda hili, bali Yesu Kristo mwenyewe anakwenda kuhusika na ninakuhakikishia utatoa ushuhuda mzuri wa ushindi baada ya maombi haya.

Wewe mwenyewe utakwenda kuyasoma maombi haya, ni maombi yenye nguvu na uwezo wa Mungu (Yehova); kwa imani gusa kioo cha kompyuta yako, simu yako au kitu chochote unachotumia kufuatilia somo hili:-

Toba: Ee Yesu Kristo nasogea mbele zako mimi na nafsi yangu, ninaomba unisamehe dhambi zangu zote, unitakase kwa damu yako ya thamani iliyomwagika pale msalabani kwa ondoleo la dhambi za wanadamu. Ulifute jina langu katika kitabu cha hukumu na uliandike katika kitabu chako cha uzima. Amina.

 

MAOMBI: Mungu Baba katika jina la Yesu Kristo, ninamleta mtu huyu asiye na msaada wo wote zaidi yako, na imani iliyomo ndani yake kwako, msamehe makosa yake yote, umtakase na kumuosha kwa damu ya Yesu Kristo. Ninafuta kila laana na mikosi katika misha yake, iliyosababishwa na kila namna ya sababu, ninatamka baraka na ushindi katika maisha yake yote, yeye mwenyewe, familia yake na uzao wake wote unakwenda kubarikiwa sasa, mifugo yake, kazi za mikono yake, mashamba yake na nyumba yake, vyote vikabarikiwe sasa, kwa jina la Yesu Kristo. Amina.

Post a Comment

0 Comments