NCHI YA UKOMBOZI MINISTRY
HATUA 12 ZA KUOMBEA HALI YA KIROHO YA
ARDHI ILI UFANIKIWE KIMAISHA.
Ukipita
mitaa mingi utakuta kuna nyumba nyingi hazijakamilika kujengwa, kuna wengine
wamekamilisha kujenga kabisa lakini wanashindwa kukaa ndani yake, mtu kama huyu
unamuombeaje? Tutapitia hatua kadhaa hapa.
HATUA YA KWANZA
1. PELEKA OMBI HILO KWA MUNGU (IWE NI
WEWE MWENYEWE AU HITAJI LA MTU MWINGINE)
Mtu akileta
hitaji lake kwako sio kwamba hana Mungu, bali anahitaji msaada wa maombi kutoka
kwako. Sasa Mungu anaweza akakusemesha moja kwa moja wakati huyo anakuambia
hitaji lake au akakusemesha mapema kabla hajaja. Muhimu fikra zako zifikiri
kuwa hilo jambo unalipeleka kwa Mungu kwa eneo ulipokwama kimafanikio.
HATUA YA PILI
2. POKEA NENO LA MUNGU UNALOPEWA NA
MUNGU KWA AJILI YA HUYO ANAYEOMBA UMWOMBEE
Zaburi
107:19 - 20 “Wakamlilia BWANA katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao.
Hulituma neno lake, huwaponya, Huwatoa katika maangamizo yao.”
Isaya 55:11
“ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia
bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”
Hapo utaona
kuna neno la Mungu ambalo ndani yake kuna wazo la Mungu ambalo lina mkakati wa
Mungu ambalo ndani yake kuna mvua inayotakiwa kuotesha. Ikimaanisha kila neno
linalokuja ndani yake kuna upako wake na linahakikisha linafanikiwa katika lile
lilokusudiwa.
Watu wengi
wanafikiria maombi peke yake yatawafanikisha, hapana, maombi yanabeba mahitaji
yako kwa Mungu na Mungu akitaka kukufanikisha atakupa neno. Ndio maana ni
hatari sana unapoenda kanisani, unahitaji maombi na sio neno. Au unafika kwenye
mkutano muda wote unawaza ataomba saa ngapi lakini hutaki kukaa chini ili
usikilize neno.
Ni gharama
kubwa kwako kuishi ukitegemea maombi kwa sababu ni maisha yasiyo na mafanikio.
Maombi yanabeba mahitaji toka kwako kwenda kwa Mungu, neno linabeba majibu
kutoka kwa Mungu kuji kwako. Ni mawasiliano ya njia mbili, na sio Mungu
akusikilize wewe tu.
Yesu alisema
katika Mathayo 4:4 “Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate
tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” Usije ukabadilisha
sehemu ya neno ukaweka maombi kwa sababu maombi peke yake hayawezi
kukufanikisha. Jaribu kutafuta waombaji wazuri halafu ona na maisha yao. Nchi
inaweza ikawa na waombaji wazuri sana lakini wasipokuwa na neno la Mungu
hawatakuwa na maendeleo. Pia viongozi wasiopokea neno la Bwana katika nchi yao,
wasahau kuwa na maendeleo kabisa.
Hii ni sawa
na mtu ambaye mvua imenyesha lakini amesahau kutafuta mbegu za kupanda na
anasubiri mavuno, na ukimuuliza anakuambia mvua ilinyesha. Ukimuuliza ulipanda
mbegu? Atakujibu aliomba ila hajapanda mbegu. Kwa hiyo ni muhimu sana kuwa na
neno la Mungu ili likusaidie wakati wa uhitaji wako wa kimazingira, ndio maana
Mungu aliweka msisitizo kwenye neno.
HATUA YA TATU
3. OMBA MUNGU AKUPE KUSIKIA MWONGOZO
WAKE KWAKO KUTOKA KWENYE NENO ULILOPEWA NA MUNGU KWA AJILI YA KUMWOMBEA HUYO
MTU AU WAKATI ULIPOJIOMBEA MWENYEWE
Warumi 10:17
“Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo.” Kuna
kusikia sauti ya neno, na hiyo sauti ndiyo inakutengenezea uhakika ambao
unakupa imani. Sawasawa na Waebrania 11:1 na Waebrania 11:3“Imani haiji kwa
neno, bali huja kwa kusikia.”
Haijalishi
ni imani ya namna gani. Imani yako kwa mganga wa kienyeji au kwa hospitali
fulani na daktari fulani zote zilikuja kwa kusikia. Sasa ili ujue ni imani ya
namna gani, lakini lazima ujue ulisikia kwa namna gani. Kama ni imani kwa Mungu
kupitia Yesu Kristo lazima utasikia kwa kuletwa na neno lake.
Imani humpa
mtu ufahamu na kujua kwa hiyo utajua namna ya kuomba ipasavyo ili uweze kutoka
mahali ulipo. Ndio maana hiki kipengele cha tatu ni cha muhimu sana kuwa Mungu
akupe kusikia kutoka kwenye neno ulilopewa ili imani yako ijengeke na uje
ufanye nini.
Tuangalie
mfano hapa. Kumbukumbu la Torati 8:7, 11-12 “Kwa kuwa BWANA, Mungu wako,
yuakuingiza katika nchi nzuri, nchi yenye vijito vya maji, na chemchemi, na
visima, vibubujikavyo katika mabonde na milima; Jihadhari, usije ukamsahau
BWANA, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake,
ninazokuamuru leo. Angalia, **utakapokuwa umekula na kushiba, na kujenga**
nyumba nzuri na kukaa ndani yake;”
Anapozungumzia
ujenzi na kuhusisha na ardhi inamaanisha anazungumzia kumwingiza huyo katika
nchi. Nchi maana yake ni ardhi yenye mipaka halali ya kiumiliki.
Maana yake
anampa eneo la kujenga kwa hiyo kuna suala la kumiliki ardhi kihalali kiroho na
kimwili kabla ya kujenga. Kwa mfano wale wanaojenga karibu na barabara
wasisahau kuwa barabara ina haki kuliko wao. Barabara ikiamua kupita, utaipisha
tu haijalishi umejenga nini hapo.
Katika
misingi sheria ya nchi mbalimbali, sheria ya barabara ina nguvu kuliko sheria
ya kumiliki kwako nyumba. Barabara iko tayari ikulipe ili utoke kwenye njia
hiyo na kuna muda wanajua kuwa barabara itapanuka patawekwa na eneo la akiba ya
barabara sasa nawe usijifanye mjanja ukajenga huko. Haya mambo yote yapo kwenye
Biblia ila nitakuonyesha pole pole.
Mungu
anapowaambia kuwa atawaingiza katika nchi, kabla kisheria haijawa ya kwao
kimwili, ilikuwa ya kwao kwa jinsi ya sheria kiroho.
Agano ni
sheria mama ya sheria zote. Ni sawa na katiba ambayo ni sheria juu ya wananchi
wote walioko katika mipaka hiyo ya kiutawala. Sasa kiroho kuna kitu kinaitwa
agano la Mungu au la miungu ambayo ni sheria mama inayobeba sheria ndogo ndogo
kuweko na ndani yake inakuwa na vipengele vya ardhi.
Hakuna agano
lolote lisilo na kipengele cha ardhi. Ndio maana Mungu anasema utakapokuwa
umekula na kushiba, na kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake;”
Kwa hiyo
kuna suala la kujenga na siyo kujenga tu bali hata kiwango cha ujenzi huo
inapaswa iwe nzuri. Je nyumba nzuri ni ipi? Wewe unaweza ukasema hiyo nyumba ni
nzuri lakini Mungu anaona sio nzuri. Maana yake kuna kiwango fulani cha nyumba
za watu wake alizoziweka.
Si suala tu
la kujenga nyumba au barabara bali ni kwa kiwango kipi cha ubora ambacho nyumba
hiyo au barabara hiyo imejengwa? La sivyo baada ya miaka michache
imeshaharibika.
USHUHUDA
Wakati
fulani tulienda kwenye shule ya msingi ambayo mke wangu alisoma zamani.
Tulipoenda kuangalia jengo la darasa la kwanza na la pili tukakuta kilichoanza
kubomoka ni milango. Madawati yalikuwa yamebaki machache sasa. Cha ajabu
tuliona ukutana na sakafu bado vikiwa imara.
Walimu
walioko pale wakatupeleka kwenye darasa lingine ambalo ndio limemaliza miaka
miwili tangia limejengwa. Na sakafu na ukuta wake ulikuwa umeanza kutoboka
toboka. Fedha zilizotumika kujenga jengo hilo lililotimiza miaka miwili ni
kubwa sana kuliko fedha jengo la zamani.
Suala la
ubora wa jengo ni suala la kiroho kabla halijawa la kimwili. Sasa anazungumza
suala la kukaa ndani yake. Haupaswi tu kujenga bila kukaa ndani yake lazima
utumie hilo jengo vizuri.
Kwa hiyo
kuna umuhimu wa kusikia kwenye mistari ya Biblia unayosoma kila mara.
Utakapoomba kwa Mungu kuwa kwa nini umekwama katika ujenzi, Mungu atakujibu kwa
kutumia neno kwa kukupa mistari iliyoko kwenye Biblia kwa sababu imani na mbinu
yako inajengeka hapo. Ukikosea hapo (kwenye misingi) utapata wakati mgumu sana
la sivyo uombe kwa kunena kwa lugha ili Roho Mtakatifu akusaidie kuomba (Warumi
8:26). Pia Roho Mtakatifu anaweza akakupa neno ili ujue mahali pa kukanyaga.
Kwa hiyo
Mungu anapokupeleka katika eneo fulani anajua unatakiwa kukaa hapo kwa muda
gani sawa na vile alivyowaambia wana wa Israeli kuwa watakapofika Babeli
wajenge kwa sababu watakaa muda mrefu kwa sababu hakuwa na mpango wa kuwaondoa
haraka (Yeremia 29).
Mungu
akishakupa uhamisho atakuambia na la kufanya, mojawapo ni kukuambia ujenge
nyumba yako ili ukae kwani sio mpango wa Mungu ukae kwenye nyumba ya kupanga.
HATUA YA NNE
4. OMBA MUNGU AKUPE KUTAMBUA MASHARTI
YA KIROHO YALIYOPO KWENYE ARDHI UNAYOKUSUDIA KUJENGA AU UNAYOJENGA JUU YAKE
Ukisoma tena
ile Kumbukumbu la Torati 8:7, 11-12 utaona cha msingi kukumbuka ni kuwa kuna
suala la kufahamu masharti ya kiroho ya ardhi hiyo unayotaka kujengea au ya
yule mtu anayetaka kujenga. Katika kumiliki kuna umiliki wa kisheria wa kiroho
kwanza kabla haujawa umiliki wa kawaida.
Sheria za kiroho za ardhi zina nguvu
kuliko sheria za kimwili za ardhi.
Maana yake
unaweza ukahalalishwa kwa sheria za kimwili kumiliki ardhi, sheria za kiroho
zikakunyima uhalali. Na sheria za kiroho zikikunyima nafasi huwezi ukakata
rufaa kule sheria za kimwili zinapowekwa lazima uende kwa aliyeweka sheria za
kiroho.
Sasa kwenye
mistari hiyo hapo juu, Wanaisraeli walipewa agano zito sana ambalo Mungu
alifunga na Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Hawakupewa ardhi tu kwanza bali Mungu
alichukua kwanza ile ardhi ikawa ya kwake kisheria. Ndio maana Biblia inasema
na wao wasipokaa vizuri kule, walioko pale na wao wataondolewa kwa sababu
hawajakaa sawasawa na sheria na taratibu alizojiwekea Mungu ili wapate kuenenda
(ardhi itawatapika) kwa hiyo walioko pale wanatakiwa wafuate sheria na taratibu
zote za Mungu.
Ishmaeli
alibarikiwa na Mungu kwa sababu ni mtoto aliyetoka katika viuno vya Ibrahimu
lakini alibarikiwa nje ya agano. Wakati Mungu anamwambia Ibrahimu, Ishmaeli
alikuwa ameshazaliwa na Ibrahimu akajitetea kuwa Mungu ambariki Ishmaeli kwa
sababu Ibrahimu na Sara wanaona hali zao haziruhusu wao kupata mtoto hata kwa
mwaka unaofuata.
Ndipo Mungu
akamwambia kumbariki Ishmaeli atambariki, lakini agano lake atalifanya imara na
Isaka. Kwa hiyo inamaanisha kuna baraka ndani ya agano na kuna baraka nje ya
agano. Kitu kimojawapo ambacho kipo ndani ya agano ni umiliki wa ardhi ambayo
Mungu aliyeweka agano, anawamilikisha watu anaotaka wabarikiwe kuliko wengine,
kihalali.
Ishmaeli na
uzao wake walibarikiwa lakini hawakupewa ardhi ya Ibrahimu, na Isaka na Yakobo.
Wakati Ibrahimu alipokufa na anazikwa, walikuwepo wake zake rasmi wawili na
masuria zake. Mke wa kwanza rasmi ni Sara na wa pili baada ya Sara kufa aliitwa
Ketura na alikuwa na watoto watano (Mwanzo 25:1-6).
Katika mgawo
Isaka alipewa ardhi, Ishmaeli hakupewa hata watoto wa Ketura hawakupewa. Baada
ya Ibrahimu kufa watoto wa Hajiri walielekea eneo tofauti na pale walipokuwepo
mwanzoni. Haki mojawapo ya mwananchi wa nchi fulani ni juu ya umiliki wa ardhi,
wageni hawawezi wakamiliki ardhi kirahisi rahisi. Ardhi ni sehemu ya baraka
katika nchi husika na katika ulimwengu wa roho ni vivyo hivyo. Wale ambao Mungu
amewakusudia hao ndio wa muhimu kumiliki eneo hilo kuliko wanaokuja.
Wana wa
Israeli wakati wanaingia katika nchi ya Kanaani walikuwa chini ya sheria ya
kumiliki na kukaa kwenye ardhi ile. Watu wengi sana wanashindwa kumiliki au
wanashindwa kujenga nyumba nzuri kwenye ardhi ile kwa ubora unaotakiwa kwa
sababu ya kukiuka masharti ya kiroho yaliyoko kwenye ardhi.
Yoshua 6:26
“Naye Yoshua akawaapisha kiapo wakati ule, akasema, Na alaaniwe mbele za BWANA
mtu yule atakayeinuka na kuujenga tena mji huu wa Yeriko; ataweka msingi wake
kwa kufiliwa na mzaliwa wa kwanza wake, tena atayasimamisha malango yake kwa
kufiliwa na mtoto wake mwanamume aliye mdogo.”
1 Wafalme
16:34 “Katika siku zake, Hieli Mbetheli akajenga Yeriko; akatia misingi yake
kwa kufiwa na Abiramu mzaliwa wake wa kwanza, na kuyaweka malango yake kwa
kufiwa na mwana wake mdogo Segubu; sawasawa na neno la BWANA alilolinena kwa
Yoshua mwana wa Nuni.”
Ukipewa huu
mstari kwa ajili ya wanaoshindwa kujenga nyumba au kushindwa kumiliki ardhi
ujue kwenye msingi na malango kuna kiapo cha laana kinachotakiwa kishughulikiwe
kwanza. Sasa kwa sababu Roho Mtakatifu yuko ndani yako atakupa uzito ndani ya
moyo wako muda ambao unataka kujenga hapo ili uingie katika maombi.
USHUHUDA
Mtu mmoja
alikuwa anajenga nyumba yake na ilifika hatua nzuri sana, ilifika mahali
hasogei kabisa kwa sababu pesa iliisha kabisa hadi ndoa yao iliingia mgogoro na
hawakujua kitu cha kufanya. Nikiwa kwenye mkoa wao wakanieleza shida yao na
wakataka niende kwenye hilo eneo na tulipoenda kwenye eneo hilo tulipoingia
getini wakauliza sasa tutaanzia wapi, nikawaambia wakae pembeni kwanza ili
nikaombe.
Nikazunguka
na kuingia ndani na nikaanza kuomba kumwuliza Mungu kwa nini wale watu
wamekwama kwenye ujenzi huo? Ghafla huo mstari ukaja na nikamwita mwenye nyumba
kuwa anioneshe mahali walipokuwa wanaingilia kwa gari au miguu kabla
hawajajenga ule ukuta. Tulipofika pale nikawaambia pale ndipo penye lango na
kuna kitu kipo pale na kinapambana na wao, kwa hiyo tukaombe.
Ndipo
tukashikana mikono tukaomba kuvunja laana katika lango lile na kinazuia wale
watu kujenga. Wakati tunaomba Mungu akanioneshea mifupa, nikafungua macho na
kuwauliza kuwa wakati wanachimba msingi wa ukuta huo walikuta mifupa ya watu?
Wakasema ndio.
Wakanionyeshea
mahali hapo tukaomba hapo, wakamalizia kujenga nyumba yao na sasa wanakaa
kwenye hiyo nyumba yao. Hivi ni vitu halisi na usipojua unaombaje utasumbuka
sana. Kiapo cha laana hakikuachiliwa kwenye eneo lote la nyumba hiyo bali
kiliachiliwa kwenye misingi tu na kwenye lango. Lazima ujue kila kiwanja kina
misingi na kina mlango na isimfungulie katika ulimwengu wa roho kila mtu
anayeingia hapo.
Mungu akupe
kuona masharti yaliyoko mahali hapo. Kwa mfano unapewa Mwanzo 28 : 10 - 20,
Hapa kuna habari za Yakobo kulala katika eneo linaloitwa Luzu baadaye akapaita
Betheli baada ya kugundua ya kwamba pale ni malango ya mbinguni kwa kuona
kwenye ndoto, malaika wakipanda na kushuka. Halafu Mungu akajifunua na kusema
nchi au ardhi alipolala Yakobo, ina umiliki wa kiroho (sio ya kawaida) na
atampa yeye sawasawa na agano la Mungu na Ibrahimu na Isaka.
Ukipewa
mistari ya namna hiyo na haisemi kitu cha kujenga pale inamaanisha Mungu
anajaribu kusema ardhi ile ina madhabahu ya Kimungu na inamilikiwa na Mungu kimkataba/kiagano.
Iwe ni Mungu huyu tunayemwabudu katika Kristo Yesu au miungu mingine ila ardhi
tayari ilionesha ina madhabahu. Lazima mtu ajue pale kuna mlango wa kiroho na
haitakiwi kujenga tu.
USHUHUDA
Tulikutana
na mchawi mmoja kwenye mkoa mmoja alitueleza anavyofanya akiwa chumbani kwake.
Kuwa alikuwa anapiga filimbi, ardhi inapasuka halafu anapotelea huko ili aende
kuzimu (ninyi hapo mtafikiri kuwa yupo ndani kumbe ameshaondoka). Sasa
alipotumwa kwenye semina yetu kuja kuloga, alikamatwa na Yesu Kristo na
akaishia kuokoka na sasa ni mchungaji.
Alitusimulia
vitu hivyo lakini kwenye Biblia vitu hivi vipo. Na Yakobo anasema kuwa kumbe
pale ni nyumba ya Mungu (mahali Mungu ameamua kukaa na hana mpango wa kuondoka)
na pia ni lango la mbinguni. Sasa kama ni Mungu wa kwako na ndio anamiliki hilo
eneo halafu wewe ndio unatafuta labda utumie hirizi pale lazima uumie.
Marko 5 : 1
- 17 inazungumza habari za Yesu kwenda katika mji wa Wagerasi na kumkuta yule
anayekaa makaburini, akamfungua na akapona. Yule mtu alipona baada ya
kuhakikisha kwamba nguruwe wameenda kwenye ziwa yule mtu akapona. Wale wafugaji
wa nguruwe wakakimbia kwenda kwenye kijiji chao na kueleza habari ya mambo
yaliyotokea na kijiji kizima kikaenda pale wakakuta yule mtu miguu pa Yesu na
ni mzima kabisa.
Hofu
ikawaingia watu wote sasa wakamwomba Yesu aondoke katika mipaka yao; hawana
shida na Yesu anayekuja kwenye mipaka yao bali wana shida na Yesu anayebaki
kwenye mipaka yao.
Lile neno
mipaka lina maana kubwa sana ndio maana hata yale mapepo yaliyojiita jeshi
yaliomba asiwaondoe kwenye lile eneo walijua katika ulimwengu wa roho Yesu ana
sheria kubwa ambayo inaweza ikawaondoa mapepo kwenye eneo lile.
Yesu naye
alijua utaratibu na sheria ya kwamba yale mapepo hayakuingia vivi hivi, lazima
kuna chanzo iwe ni ardhi ya pale au wenyeji wa pale ndio walitoa mipaka yao kwa
nguvu za giza. Yesu akatii ile shuruti na akaondoka katika mipaka yao. Na
alipofika ng'ambo ya pale kuna wengine walikuwa wanamsubiri ili awahudumie.
Wewe unanunua
kiwanja kwenye eneo fulani ambapo mipaka yake ipo chini ya himaya ya mungu
mwingine halafu unafika pale na Yesu wako bila kushugulikia sheria itakayoondoa
mapepo hapo halafu ukabaki na sheria inayosema Yesu akifika aondoke katika
mipaka hiyo.
Mwingine
ananunua kiwanja halafu anawaambia watu wa nyumbani kwake na kuwaambia waende
pale kumshukuru na wanafika na kuomba kuweka wakfu kwa Mungu, siku inayofuata
mwenye kiwanja anakuja na kusema amebadilisha mpango, uchukue hela yako.
Saa nyingine
unapanga nyumba sehemu halafu unaanza kumshukuru Mungu na kumkaribisha Yesu
akae mahali hapo. Hujui misingi na mipaka ya hiyo nyumba angalia baada ya mwezi
kidogo wakiona hawana namna ya kukufukuza unapandishiwa kodi kubwa kabisa.
Halafu unatishiwa kuwa usipolipa ndani muda huo unafukuzwa lakini kwa wengine
hazungumzi kitu chochote nawe unabaki kujiuliza.
Shida yako
ni kwamba umemkaribisha Yesu; hawana shida na wewe bali na Yesu uliyemleta.
Sasa hawawezi kumfukuza Yesu bila wewe kwa hiyo na wewe lazima uondoke tu ili
na Yesu wako aondoke. Iko sheria iliyoko juu ya sheria ndio maana kuna mahakama
ya rufaa yaani kuna mtu anaweza akapangua hukumu iliyowekwa.
Ukisoma
Ezekieli 45:1,4 utaona neno patakatifu. Patakatifu maana yake ni eneo
lililotengwa kwa ajili ya Mungu. Kazi yake ni mahali watajenga makuhani,
watajenga pa kufanyia ibada yaani patakatifu pa patakatifu.
Unganisha na
Ezekieli 48:8, 10, 14 “Na mpakani mwa Yuda, toka upande wa mashariki hata
upande wa magharibi, yatakuwapo matoleo mtakayotoa, upana wake mianzi ishirini
na tano elfu, na urefu wake sawasawa na moja la mafungu hayo, toka upande wa
mashariki hata upande wa magharibi; na mahali patakatifu ni katikati yake.
Matoleo hayo matakatifu yatakuwa kwa watu hawa, kwa makuhani; upande wa
kaskazini urefu wake ishirini na tano elfu, na upande wa magharibi upana wake
elfu kumi, na upande wa mashariki upana wake elfu kumi, na upande wa kusini
urefu wake ishirini na tano elfu; na mahali patakatifu pa BWANA patakuwa
katikati yake. Wala hawatauza sehemu yake, wala kuibadili, wala hawatawapa
wengine malimbuko ya nchi; maana ni matakatifu kwa Bwana.”
Ukisoma mistari
yote ya Ezekieli 48:8 - 14 utapata maelezo mazuri zaidi. Hapo utaona ardhi
imezuiwa kuuzwa kisheria katika ulimwengu wa roho halafu wewe unanunua bila
kujua masharti yake lazima utapoteza hela yako bure. Aliyezuia kuuza ni Mungu
au mungu anayemiliki mahali hapo.
Kama eneo
limeuzwa kwa miungu na huna namna ya kuyabandua hayo mapepo mahali hapo katika
mapatano ya namna hiyo kwa kufanya shughuli zao na kutolewa sadaka ujue hilo ni
zuio katika ulimwengu wa roho.
Ukianza
kuomba Mungu atakupa mstari kama huo ili ujue kuna zuio katika ulimwengu wa
roho na ametaka kujua Mungu anataka ulimiliki la sivyo utapata shida sana.
USHUHUDA
Mtu mmoja
alipata eneo la kujengea nyumba yake na mahali alipopata ni eneo la mlima. Sasa
alipoanza kujenga mafundi wanajenga vizuri kabisa lakini sehemu iliyojengwa
kesho yake wanakuta imebomolewa na hali hiyo ikatokea siku kadhaa. Ndipo
wakaenda kwa wenyeji kujua labda kuna watu sio wazuri na wanawafanyia fujo.
Wenyeji
wakasema hakuna anayewafanyia fujo bali ule mlima ni wa miungu, hautolewi vivi
hivi una masharti. Kama mtu anataka kuchukua lazima mapatano ya amani yawepo
kwa kutoa sadaka.
Sasa yule
mtu akasema yeye ni Mkristo kwa hiyo hawezi akatoa hiyo sadaka. Wale wenyeji
wakasema sio lazima yeye atoe bali awape wao hiyo pesa halafu wao watatoa.
Akakubali na kuwapa hela ya sadaka hiyo. Hao wenyeji wakatafuta ng'ombe na
kufanya taratibu zingine za kwao wakatoa sadaka ili miungu ya ule mlima
imkubalie yule mtu kujenga.
Baada ya
kumaliza wakampa taarifa yule ndugu kuwa miungu imekubali sadaka yake sasa
anaweza kuendelea kujenga. Akapeleka tena mafundi wakajenga kuanzia siku ya
kwanza mpaka alipomaliza ule ujenzi, nyumba haikubomoka. Lakini baada ya pale
aliugua. Sasa utajiuliza kwanini aliugua? Pia alifikilisika kabisa. Wakati namwombea
Mungu akanipa hii mistari nikapata ufahamu ndipo nikaanza kumhoji maswali
akanieleza kila kitu. Nilipaswa kupata ufahamu wa ki-Mungu ili kumsaidia hapo.
Watu wengine
walijenga kabla hawajaokoka au wengine hawajajenga kabisa ingawa wana viwanja, au
wanaanza kujenga ila hawamalizi au wanajenga ila hawakai ndani yake. Sasa kuna
haja ya kufuatilia hili somo kwa mfululizo unaofuata ili tuone kwa undani namna
ya kupata msaada wa Mungu kukuokoa.
HATUA YA TANO
5. MUULIZE ALIYEHITAJI KUOMBEWA IKIWA
AMEWAHI KUTAFUTA KUPATANISHWA KIROHO NA KUFUATA MASHARTI YALIYOPO KATIKA ARDHI
ANAYOJENGA
Ukisoma 2
Wafalme 17:24–29 utaona mfalme wa Ashuru alipoenda kupambana na mfalme wa
Israeli. Na akashambulia eneo la Samaria na alishinda. Kwa hiyo alichofanya
aliwahamisha wa Israeli walikuwa kwenye mji wa Samaria na kuwapeleka kama
mateka alikowapeleka. Na badala yake aliwaleta watu wengine ambao wametajwa ya
kwamba ni watu kutoka Babeli, na Kutha, na Ava, na Hamathi, na Sefarvaimu na
kuwaweka kwenye Mji wa Samaria badala ya wana wa Israeli.
Biblia
kwenye mistari hiyo inasema Mungu wa nchi, maana yake ni Mungu anayemiliki
ardhi yenye mipaka halali (maana nchi ni ardhi yenye mipaka halali). Ni Mungu
mwenye umiliki kiroho juu ya hilo eneo wanalokaa na ana watumishi wake wanaojua
taratibu na sheria za kiroho juu za hiyo ardhi wanaoitwa makuhani.
Na ndiyo
maana mfalme aliagiza makuhani hao wakaletwe na kupelekwa kukaa kule Samaria na
kuweza kuwaeleza wenyeji walioshindwa kukaa kule kawaida ya Mungu wa nchi ile
ili wasije kumalizwa na simba. Maana hawa watu walikuwa hawamwabudu huyu Mungu
lakini walilazimika kupatana naye, wafuatane masharti yake juu ya ardhiili
wakae salama.
Sasa basi
ile kwamba mtu amehama basi haina maana Mungu wake amehama. Na ndiyo maana
lazima uwe mwangalifu kuuliza kwanza juu ya kiwanja unachonunua je huyo mtu
alikuwa nani au ni nani aliyekaa kabla yako kwenye hiyo nyumba ya kupanga. Na
hii ni kwa sababu wengine wanapokuja kukaa huwa wanakuja na miungu yao na
kuikabidhi yale maeneo na wanapohama hawahami na miungu yao wanaiacha hapo hapo
na mtu mwingine atakayekuja kumiliki hilo eneo kama mgeni atakutana na masharti
ambayo yanatoka kwa mungu mwingine ambaye si wa kwake. Na hampi kibali cha
kuendelea kukaa kwa amani kwenye eneo hilo bila kujua masharti na kuyatimiza.
Kwa hiyo unapofika
mahali kwa kukabidhi ardhi kwa miungu mingine halafu roho yako na mwili wako
umeukabidhi kwa Mungu aliye hai ni kujitafutia ugomvi kwenye hilo eneo
unalokwenda kulala na kujenga hapo na huo ugomvi hutaweza kujua namna hata ya
kuwa refa. Usitegemee utalala vizuri kwa sababu hiyo miungu lazima itapigana tu
na Mungu aliye hai na ikipigana ni lazima tu utapata shida. Na ndiyo maana watu
wengi sana ukiwauliza swali la namna hii au watakufika au hawatakujibu au
hawatakujibu vizuri. Lakini ukikaa vizuri na Roho Mtakataifu atakupa ufahamu
juu ya eneo hilo.
HATUA YA SITA
6. OMBA TOBA KWA MUNGU KWA AJILI YA
MAENEO YAFUATAYO:-
KWA KUVUNJA NA KUTOFUATA MASHARTI YA
MUNGU YANAYOHUSU ARDHI INAYOTUMIKA KUJENGA. NA HII NI PAMOJA NA KUCHANGANYA
MIUNGU — KWA KILICHO SABABISHA SHETANI AKAPATA NAFASI YA KUMILIKI ENEO NA
KUWEKA MASHARTI YAKE.
Ukisoma
Danieli 9:16 na Maombolezo 5:7 utaona hili ni suala la kisheria la ki-Biblia la
msingi sana. Wazee watu wakifanya dhambi sisi hatuchukui dhambi zao bali
tunachukua maovu yao yanayotokana na dhambi walizofanya. Kwa hiyo unatubu kwa
ajili ya dhambi zako, bali huwezi kutubu kwa ajili ya dhambi za baba au babu
zako. Bali unatubu kwa ajili ya uovu wa baba au babu zako.
Kwa mfano
Malaki 1:3–4 Anazungumza juu ya watu wawili hapa Esau na Edomu. Sasa ngoja
kwanza tuwajue hawa walikuwa ni watu wa namna gani, tusome kile kitabu cha
Mwanzo 36:40,43 Kwa hiyo Biblia inapozungumza kwenye Malaki inasema
“nimemchukia Esau na kwa sababu hiyo mahali pale pamekuwa ukiwa na nimepazuia
pasijengwe na sehemu yake nimewapa mbweha wa nyikani, nimemzuia asijenge”.
Sasa mtoto
wake Edomu anasema pamoja na kwamba tumepondwapondwa na hali zetu za kimaisha
sina shida tutajenga. Ni mtoto akisema hayo mahali ambapo baba yake alishindwa
kupajenga baada ya kubomolewa.
Na Mungu
anasema wakijenga atabomoa. Kosa la baba aliyekutangulia hapo lakini sasa baba
amekufa hajajenga maana alichojenga kilibomoka. Sasa kiwanja kakuachia na wewe
unataka kujenga bila kujua kilichosababisha kubomolewa kwa kile alichojenga. Pamoja
na kiwango kidogo cha pesa ulichonacho ukishajenga Mungu anakuja kubomoa. Na
ndiyo maana wako wengi tu walioachiwa viwanja na mashamba na baba zao lakini
wameshindwa kujenga. Au wana nyumba ambazo wameshindwa kuzimalizia ambazo
wazazi wao walianza kujenga na kuishia katikati au walijenga zikabomoka.
Na hii yote
ni kwamba bila toba huwezi kujenga. Hapawezi kujengeka na si kwamba shetani
anazuia bali ni Mungu anayezuia si kwa ajili ya ajili yako bali kwa ajili ya
baba zako.
HATUA YA SABA
7. OMBA MUNGU AONDOE MAZINGIRA YA
UKIWA ILI ZUIO LA KUJENGA LIONDOKE NA MADHARA YAKE KWAKO/AU KWAKE YEYE
UNAYEMUOMBEA YAONDOKE/YAKUACHIE/YAMUACHIE UNAYE MUOMBEA
Ukisoma
Ezekiel 35:9 Kwa hiyo tafsiri moja ya ukiwa ni watu kutokukaa kwenye hilo eneo
lenye ukiwa. Ukiwa unaondoa watu wasiweze kukaa hapo.
Pia ukisoma
Isaya 5:9 utaona ya kwamba kule kwenye Ezekeli tumeona ya kwamba Mji hautakuwa
na watu. Na hapa kwenye Isaya imelenga moja kwa moja kwa watu waliokwisha
maliza kujenga nyumba na nyumba zao ni nzuri lakini hazina watu. Ukiwa unazuia
na kuondoa mpaka wapangaji na hata watu wa kukodisha.
Lakini pia
Ezekieli 33:28 inasema Eneo lenye ukiwa hata mtaani unaweza usione watu,
hawalitembelei wala kwenda eneo hilo.
Na ukisoma 2
Samweli 13:20 utaona ya kwamba Tamari alikaa kimaombolezo na uchungu uliomfanya
awe mzito kutoka ndani ili kufanya kazi nje na kujishughulisha na mambo
mengine. Ukiwa huwa unakufurahisha kukaa ndani hata kama huna kazi. Ukiwa
unakuhalalisha kutokufanya kazi hata kutokutoka nje.
Kule kwenye
Malaki 1:4 tulikosoma utaona ya kwamba ukiwa unazuia ujenzi. Ukiwa aliopewa
Esau ulizuia ujenzi. Na ndio maana Edomu alipotaka kujenga ukiwa ulitoa uhalali
wa kubomoa kilichojengwa kwa sababu kimejengwa wakati kuna zuio. Na kile kitabu
cha Amosi 6:11 kinasema Ukiwa unasababisha na kutegeneza mazingira ya nyumba
kubomoka na kupigwa na ufa ili isikaliwe kabisa.
Hata
ukiongezea kusoma Yeremia 51:26,29 utaona ya kwamba kama unajenga nyumba na
kunakuwa na jiwe na pembeni au lile la msingi Biblia inasema utazuiwa. Kutakuwa
nakizuizi fulani. Unaweza kuwa na kiwanja na kuchimba mitaro kabisa lakini
nyumba yako itakwamia kwenye msingi. Na hii ndiyo gharama ya ukiwa.
Na
ukimalizia kusoma Ezekieli 15:8 kwa hatua hii utaona ikisema kwa maana nyingine
anasema “Nami nitaifanya ardhi yenye mipaka halali kuwa ukiwa” kwa hiyo ukiwa
ni matokeo ya kukosa. Na ndiyo maana baada ya kuomba toba cha msingi
kinachofuata ni KUOMBA MUNGU AONDOE ZUIO KWA SABABU KINACHOZUIA NI UKIWA
HATUA YA NANE
8. VUNJA NA ONDOA LAANA ILIYOPO
KATIKA ARDHI YA ENEO LA UJENZI
Hii
itakusaidia sana kama ulipokuwa ukiomba Mungu alikupa mstari unaofanana kwa na
ule wa Yoshua aliposema ataachilia laana kwa mtu yeyote atakayejenga Yeriko,
atakayejenga malango na kuta basi watoto wake watakufa wa kwanza na wa mwisho.
Ukisoma
Yoshua 6:26 na hata ule wa kitabu cha 1 Wafalme 16:34 kuwa haya mambo yalitokea
sawasawa na jinsi ambavyo Yoshua alisema. Kwa hiyo Mungu anapokupa mstari wa
namna hii maana yake shughulika na laana iliyopo vunja kwa Damu ya Yesu.
HATUA YA TISA
9. KEMEA ILI VIONDOKE VYOTE VILIVYOKAA
KWENYE ENEO UNALOLIOMBEA LILILOSHINDIKANA KUJENGWA AU HALIKALIKI HATA BAADA YA
KUWA UMEKWISHA MALIZA UJENZI
Kitabu cha
Isaya 13:19–22 utaona ya kwamba ukiwa ukishuka mahali si tu kwamba unazuia watu
wasikae bali unaweka zuio watu wasijenge, unaweka zuio waliojenga zibomoke na
unaweka zuio kwa wale waliokamilisha nyumba zisikalike lakini pia wale
walioamua kubaki kupoteza nguvu za kufanya shughuli mbalimbali wanakuwa mjini
lakini mji(nchi) umejaa ukiwa.
Na maandiko
yanasema kwamba ukiwa ukiingia mahali ni kama vile Mungu anakuwa anaswaga hivi
vitu yaani kuna kibali kinatolewa, linawekwa zuio na si tu zuio lakini
kinawekwa kitu kingine cha kusaidia, na maandiko yanasema “hayawani wakali wa
nyikani” Isaya 13:21a, ili ukitaka kwenda kujenga wapambane na wewe. Na Biblia
inazidi kusema “na nyumba zao zitajaa bundi; mbuni watakaa huko; na majini
watacheza huko” Isaya 13:21b.
Kwa hiyo
ukiona nyumba haijakaliwa muda mrefu unajua sasa kitu cha kufanya kwa sababu
yawezekana kuna majini yamewahi huko ndani. Kwa mfano unapoamua kununua gofu au
nyumba ambayo haijaisha usije ukafikiri liko/iko yenyewe tu.
HATUA YA KUMI
10.OMBA MUNGU AKUJULISHE IKIWA UKIWA
UMEONDOLEWA NA WAKAAJI HAO WABAYA NA WAMESHALIACHIA ENEO HILO
Hii
inamaanisha umeshafanya maombi sasa unataka kujua ya kwamba ukiwa umeondoka.
Kwanini basi unataka kujua hili? Kwa sababu ukiwa ni zuio na ni zuio
linalotumia kuzia kitu fulani na kumwambia yule mtu aliyewekewa zuio apate
kufanya matengenezo.
Sasa si kila
mahali kwenye tatizo la ardhi Mungu anatumia ukiwa kama zuio. Maana inategemea
na hii ni kutokana na mstari nilioanza nao. Kwa hiyo ukitaka kujenga kwenye
kiwanja ambacho kina zuio ni lazima kwanza uweze kuondoa zuio ili uweze
kuendelea, kwa sababu zuio liko kisheria.
Ukisoma
Yeremia 4:27–28 Biblia inasema Mungu atakupa ndani yako maombi ya kimaombolezo.
Kuna mzigo fulani utakuja ndani yako na ukiwa unakuja utakuja na kitu cha
maombolezo na maombolezo hayo yatakusukuma kuomba. Hayatakusukuma kukaa ndani
bila kufanya kitu.
USHUHUDA
Tulienda
mahali fulani kwenye eneo na tulikuwa tukitafuta kujenga kitu cha huduma kwenye
mkoa mmoja na tukapewa maeneo kama matatu manne hivi kuchagua na tukachagua
eneo moja ambalo lilikuwa kama msitu lakini lipo karibu na mjini na tulishangaa
sana kwamba watu hawajengi. Na sisi tukasema tunalitaka hilo eneo, wahusika
wakatuambia hata michoro haijachorwa na hata kupimwa halijapimwa lakini lipo
mjini. Tukasema sisi tunalitaka na tuko tayari kulipia gharama za awali za
mchoro. Wakatukubalia na tukalipa zilizokuwa halali wakachora na kuweka na plan
ya mji kwenye lile eneo.
Tukaitwa na
kwenda kwenye lile eneo na tukafanya kazi kama ninayokufundisha hapa na
tulipozunguka kwenye lile eneo tukagundua kuna madhabahu ya miungu mingine
kwenye kichuguu. Na kila baada ya muda alikuwa akitokeza nyoka mkubwa kwenye
kile kichuguu na wenyeji wa lile eneo wanakimbia na kuanza kumchezea na
kumwimbia. Na tukajiuliza sijui wanajuaje kuwa yule nyoka katoka nje. Lakini
alikuwa akishatoka tu wao wanakuja kumwimbia na kumchezea. Watu waliokuwa
wakisafisha pale wakataka kumuua wenyeji wakasema mkimuua tutaharibu mvua.
Wakatupigia
simu na kutueleza tukawaambia sasa ilikuwaje wakasema wenyeji walimwimbia na
kumchezea mpaka alipoona kafurahi alirudi tena kwenye shimo. Sasa kumbuka ni
kiwanja cha kwetu. Na wale wasafishaji wakatuuliza wafanyeje sasa tukawaambia
hilo watuachie na tukajikusanya baadhi ya waombaji na kwenda pale na tukafanya
baadhi ya vitu tunavyofanyaga halafu tukamnyamazisha yule nyoka kule kule
shimoni na kuvunja na ile madhabahu na kufungua lile eneo kwa sababu yule nyoka
ndiye aliyeweka zuio. Tulipovunja namna hiyo baada ya mwaka watu walipakimbilia
na kujaa hata kujenga. Kwa hiyo tulipopangua zuio na majirani wakapata msaada.
HATAU YA KUMI NA MOJA
11. WEKA WAKFU KWA MUNGU HILO
ENEO/MKABIDHI MUNGU KWA MAOMBI HILO ENEO
Inawezekana
kabisa umemwomba Mungu na ndiye aliyekupa hilo eneo lakini bado anataka uweze
kumkabidhi yeye kwa njia ya maombi pia. Mwambie Mungu nakupa ili eneo ni la
kwako lifunike kwa damu yako, lilinde na kulitumia jinsi unavyotaka. Ukifanya
namna hii na kuwa na nidhamu ya namna hii kwenye eneo hilo ambalo unataka
kujenga kila ukikanyaga na kusema maneno hayo ya kumkabidhi Mungu ndani yako
Mungu anakupa plan (mpango).
2 Mambo ya
Nyakati 6:12–42 Biblia inasema Sulemani alipokwisha kumaliza kujenga nyumba ya
Bwana na nyumba yake mwenyewe sawasawa na yote yaliyoingia ndani mwake moyoni
mwake kuyafanya. Sulemani aliwekewa moyoni namna ya kujenga nyumba ya Bwana na
namna ya kujenga nyumba yake. Kwa hiyo unapoweka wakfu usiweke wakfu kijumla
jumla bali weka wakfu ardhi, mipaka na kiwanja, weka wakfu misingi ya kiwanja,
weka wakfu malango ya kiwanja, ramani utakayochora mahali hapo.
HATUA YA KUMI NA MBILI
12. VISEMESHE ARDHI NA MBINGU
VISIKWAMISHE UENDELEZAJI WA UJENZI NA UTUMIAJI WA KILICHOJENGWA
Kumbukumbu
ya Torati 32:1 “Sikilizeni, enyi mbingu, nami nitanena; Na nchi isikie maneno
ya kinywa changu.” Nchi au ardhi inaweza kusikia. Kwa hiyo ni vizuri
kuitangazia kwamba zuio limeondoka. Kwa hiyo ardhi ijue kwamba ardhi hiyo sasa
ni mali ya fulani kihalali katika ulimwengu wa roho. Au kama ni wewe mwenyewe
unaiombea hiyo ardhi jifunze kuisemesha ardhi kuwa ni mali yako kwamba
isijaribu kukupinga bali yenyewe ni mali yako ambayo Mungu amekupa kwa sababu
umesha pita hatua zile nyingine zote na kukemea hata yake majini yaliyokuwa
yakikaa humo na kuwa umeshaiweka wakfu kwa Mungu na Mungu ameshatamalaki hapo.
Ukishasemesha
namna hiyo ardhi inasikia na mbingu inasikia. Na Biblia inasema Mungu anapokuja
mahali anaita nchi na mbingu na vitu vyote vinasimama kwa pamoja. Maana yake
vinategemeana. Na ndiyo maana ukisoma kwenye Biblia utakuta ikisema mbingu
kufunuka na mbingu kumfunukia. Sasa mbingu ikifunuka ni kwa ajili ya watu wengi
lakini mbingu kumfunukia mtu ni kwa ajili ya mtu mmoja au wawili au eneo.
MUNGU AKUBARIKI SANA
MAOMBI NA MAOMBEZI
PIGA: +255762756542
WHATSAP: +255762756542
0 Comments